Bukobawadau

HUU NI WARAKA MAALUM KWA WATANZANIA

MODS: Inawezekana kwamba hapa si mahala pa waraka huu, kutokana na maudhui yake. Lakini ukiangalia kwa undani, HAPA ndio mahala pake! Nawasilisha!

Ndugu Zangu Watanzania!

Nakuja kwenu leo nikiwa na waraka huu maalum ambao ni ushauri wangu wa nini kifanyike kuhusu hiki kinachoonekana kuwa mhemko au chokochoko za kidini hapa nchini. Kumbukeni, ni rahisi sana kuipoteza Amani kuliko kuirejesha. Tujihadhari, tusiangukie kwenye mikono ya Shetani, aliyelaaniwa na Mwenyezi-Mungu na kufukuzwa Mbinguni, naye akaapa kuwa Adui Namba Moja wa kila Mwanadam, yaani, kila mtu!

1. Zanzibar: Kama mnavyojionea, hali imekuwa sio shwari huko Zanzibar. Wakristo wanaishi katika hofu kuu ya kuumizwa, kuuwawa au kufanyiwa jambo lolote lile baya, wakati wowote. Nani wa kusema kwamba hali hii ikiendelea, haitafika hapa Bara? Hata kule Mbagala kuna kanisa lilichomwa moto. Lazima mkumbuke kwamba, kihistoria, vita zote mahali popote pale zilifanyika kwa sababu za KIUCHUMI! Vita Kuu ya Dunia ya Kwanza na ya Pili, zote zilifanyika kwa sababu za KIUCHUMI.

Nani walifaidika? Walifaidika waliotaka kupora mali kutoka kwa matajiri wa mataifa ya Ulaya, Mashariki ya Kati na ya Mbali, walifaidika waliotaka kutengeneza na kuuza silaha, na pia, walifaidika waliotaka kupora ardhi na kila kilichomo ndani yake. Wakati wa Vita Kuu ya Pili, mali nyingi sana (michoro yenye thamani, vito, dhahabu, fedha nyingi) zilipora nchini Ujerumani, Uswisi, Austria, Italia, Uingereza na kwingineko, baada ya wenye kumiliki mali hizo kuuwawa kwenye mashambulizi ya angani na mabomu ya kurushwa kwa makombora na mizinga!Zanzibar kuna nini mpaka kutamaniwe kiasi hicho?

Zanzibar kuna vitalu tano vya mafuta na gesi, msiniulize nani kaniambia, lakini ninafahamu na nimethibitishiwa. Kiwango cha mafuta na gesi kilichopo Zanzibar ni KINGI kuliko kilichopo hapa Bara, kwa hiyo, wenye kuyatamani mafuta na gesi wanafanya kila hila, kuvuruga amani, kwa njia ya hofu ya kidini, ili ionekane kwamba Wazanzibari sasa hawawataki Wakristo ndani ya "nchi" yao. Hilo sio kweli.

Wazanzibari wengi (ambao nimeishi nao kwa muda mrefu huko Zanzibar) ni watu wema, wenye moyo wa ukarimu, na wenye kuwapenda hata wasio Waislam.

Ndio, kuna Wazanzibari ambao (kwa kuhamia kwao huko wanaitwa Wazanzibara... kwa jina la ukweli) ambao waliondoka kwenye Ukristo na kuingia kwenye Uislam, baada ya kuishi huko kwa muda mrefu, lakini pia kuna Wazanzibari wa kuzaliwa kwenye Uislam ambao nao pia waliondoka kwenye dini hiyo na kuingia kwenye Ukristo. Iweje leo, ghafla tu, hali kama hii iingie nchini humo na kuwatia hofu kuu Wakristo, kwamba sasa hawatakiwi nchini humo?

Hizi ni Njama za Shetani, kutaka kutuchonganisha, kupitia mgongo wa mafisadi: Makuwadi wa Vita na Makuwadi wa Nishati ya Petroli.

Mwenye kuusoma waraka huu amjulishe na mwenzake, na mwenzake, ili wote muweze KUMTAMBUA SHETANI na hila zake. Tusipojihadhari na kumrejea Mungu, TUTAANGAMIA! Hakika, TUMLAANI SHETANI!


2. Uchinjaji wa Nyama kwenye Mabucha: Hivi sasa kuna ujumbe mfupi wa simu unaosambaa kwa kasi kubwa sana, ambao unadai kwamba Wakristo wote sasa, kutokana na Azimio la Kanisa (halitajwi kanisa lipi), wanapaswa kuiombea na kuitakasa nyama inayonunuliwa kwenye bucha kwa Damu ya Yesu, kwa kuwa imechinjiwa kwenye madhabahu ya Kiislam kwa kutumia majini. Uislam sasa unahusishwa moja kwa moja na mambo ya kijini, yaani, ya kishetani.Tukumbuke kwamba hali hii haikuwapo hapo awali.

Mwangalieni Shetani jinsi alivyo! Anawachochea Wakristo kupigana na Waislam, kwa njia ya kulipa kisasi baada ya Wachungaji kuuwawa na Makanisa kuchomwa moto, huku anazidi kuwachochea Wakristo kuwatenga Waislam kwa kuihusisha dini yao na Ushetani, lakini pia, anazidi kuwatia hasira Waislam kwa kuihusisha dini yao na Ushetani! Mmemuona Shetani jinsi alivyo?

Wanaosambaza ujumbe huo mfupi wa simu wanafanya makusudi wakijua kwamba watawachochea Wakristo na Waislam kuchukiana. Muislam atamchukia Mkristo kwa kuwa Mkristo amemwambia Muislam kwamba dini yake ni ya Kishetani, huku Mkristo atamchukia Muislam KWA KUWA ameambiwa dini yake ni ya Kishetani. Shetani anatupiga vita kwa kila kona. TUMWOGOPE SANA SHETANI! TUMCHUKIE, TUMLAANI, TUMFUKUZE!

Si Muislam au Mkristo atakayepona na vita hii, TUSIPOJIHADHARI!Tunachopaswa kutambua ni kwamba:


1. Kuna Waislam, sio wote, ambao wanaamini katika mambo ya Ushirikina. Sio wote. Hakuna sehemu yoyote ile ambayo dini ya Kiislam inawafundisha Ushirikina waumini wa dini hiyo. Kwa hakika, Uislam UMEHARAMISHA Ushirikina! Vitabu vyote takatifu vya Kiislam VIMEHARAMISHA Ushirikina! Vimesema: Hakika ni mwenye hasara yule yote mwenye Kumshirikisha Mungu!

2. Kuna Wakristo, sio wote, ambao nao pia wako katika imani za Kishirikina. Nguvu za giza kwao ndio somo kuu. Wanaenda kwa waganga kuomba hiki na kile, badala ya kusali na kumwomba Mungu ulinzi, usalama na msaada wake, kama ilivyoainishwa kwenye Biblia na maandiko mengine takatifu!Kwa kuwa sasa mnatambua hili, nini kifanyike?

Waislam, wameamrishwa kutamka neno "Bismillahi!" kila wanapochinja mnyama kwa ajili ya chakula, hii ina maana "Ninafanya hivi kwa jina la Mwenyezi-Mungu." Waislam hutamka hivyo pia wakati wa kula. Sikumbuki kama Wakristo wameamrishwa kumtaja Mwenyezi-Mungu wakati wa kuchinja, kwani uchinjaji wa wanyama ulianza tokea enzi za Nabii Abrahamu, ambaye wengi wetu ni wa kizazi chake. Lakini ninachojua kwamba, Wakristo husali na kumtaja Mwenyezi-Mungu wakati wa kula.

"Utamaduni" wa kuwaachia Waislam kuwa wachinjaji wa nyama ULIPOKEWA hapa nchini na dini zote, na kwa hakika, Wakristo wengi walikataa kula nyama ambayo ilikuwa HAIJACHINJWA NA MUISLAM. Wengi, wakati wakifanya sherehe za harusi, kipaimara, n.k., walisisitiza kwamba nyama itakayoliwa iwe IMECHINJWA NA MUISLAM, si vinginevyo.Imetokeaje mpaka leo ikaonekana kwamba nyama inayochinjwa na Muislam imemshirikisha Shetani kwa kupitia majini? Hamuoni kwamba HUU NI UCHONGANISHI MKUBWA wa Shetani?

Narudia tena, TUMWOGOPE SHETANI!

3. Hitimisho: Napenda kuhitimisha hapa leo kwa kusema yafuatayo:Mosi, sisi wote ni ndugu, Uzao wa Mungu kutoka kwa baba na mama yetu Adamu na Hawa. Ndio maana tukaitwa Wanadamu.Mungu alimuumba Adamu, ambaye ni mwanaume. Akampatia usingizi Adamu kisha akautoa ubavu wake mmoja na kumwumba Hawa, ambaye akamwita mwanamke, maana yake, ametokana na mwanaume.Kwa kuwa sisi wote ni ndugu, ila tuna imani tofauti za KUMWABUDU MWENYEZI-MUNGU, hakuna kati yetu mwenye HAKI ya kusema kwamba Muislam ni bora zaidi ya Mkristo, au Mkristo ni bora zaidi ya Muislam.

Sisi wote tuko SAWA MBELE YA MUNGU, kwa kuwa YEYE PEKEE ndiye mwenye HAKI ya kutukosoa na kutuhukumu. Sisi, ingawa Nabii Abrahamu alidiriki kusema na mwenyezi Mungu wakati akiwaombea watu wa Sodoma na Gomora, juu ya kwamba wakikutwa watu kumi tu ambao ni wema kwenye miji hiyo, basi wale waovu nao wasiangamizwe, hakika, Mwenyezi-Mungu amemwumba mwanadamu kwa mfano wake na amemfanya kuwa kiumbe bora zaidi kuliko viumbe wote ambao Mwenyezi-Mungu aliwaumba na kumpelekea Adamu awape majina.

Sasa, iweje leo sisi TUMUASI MUNGU, kwa kuua, kuhukumu, kuchoma moto makanisa, kuwatisha waja wake Mungu, na maasi mengine ambayo HAKIKA Shetani ametudanganya kuyafanya?Ndugu zangu, kumbukeni, kuipoteza Amani ni kuwafurahisha Makuwadi wa Vita na Makuwadi wa Nishati ya Petroli, ambao wote ni WAFUASI WA SHETANI! Hawa wanatokana na makundi ya Freemasons, Illuminati, Skulls and Bones na wengineo, ambao hufanya kazi zao kwenye maficho ya GIZA (Usiku), na si mchana kweupe, kwani mwanga wa jua la mchana unang'aa na kuleta amani, wakati mwanga wa mwezi wa usiku si mkubwa, unaruhusu kuwapo kwa Shetani miongoni mwa wanadamu.

Tafadhali sambazeni waraka huu kwa wanadamu wote waishio Tanzania, sio tu kwa Wakristo na Waislam, bali kwa Wapagani, Wahindu, Wabudhha, Wa Bah'ai, na imani zote nyingine ambazo zina waumini wake hapa nchini.

Vita ikianza, haitambagua mtu kwa imani yake.

Amani ya Bwana Wetu iwe nanyi.

Amina!


CHANZO; JAMII  FORUMS.
Next Post Previous Post
Bukobawadau