Bukobawadau

Hoja ya Nchimbi dhidi ya unyama kwa Kibanda

Na Prudence Karugendo

WAKATI  akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani, DW, kuhusu utete wa usalama unaowakumba wanahabari Tanzania, na kutakiwa ataje hatua za makusudi zinazochukuliwa na serikali kuwaondolea wanahabari zahama hiyo, Waziri wa Mambo ya Ndani, Emmanueli John Nchimbi, alitamka kwa kujiamini kwamba serikali inalo jukumu la kuhakikisha usalama wa kila raia na si kwa wanahabari peke yao.

Nchimbi aliongeza kwamba si kweli kuwa wanahabari ndilo kundi pekee ambalo usalama wake umegubikwa na utata katika jamii ya Watanzania, akasema mtu akitakiwa kutaja matukio yanayodhihirisha kuwa usalama wa wanahabari umepotea hayawezi kufika hata matukio matano. Kwa mtazamo wake mpaka sasa wanahabari wako salama! Pengine wafe nusu yao ndipo atalipa uzito suala hilo!

Lakini hatahivyo Nchimbi hakulitaja kundi lingine katika jamii ya Watanzania ambalo taaluma yake inalifanya kujikuta limepoteza usalama wake kama ilivyo kwa wanahabari. Maana kwa kuitia uzito hoja yake ya kwamba si wanahabari peke yao wanaoonekana kupoteza usalama wao kutokana na kuihudumia vilivyo taaluma yao, angeongeza walau makundi mawili yaliyo katika mkumbo mmoja kama mfano. Pengine angesema wahandisi au wahasibu. Lakini kushindwa kufanya hivyo ni kama Nchimbi kakiri kwamba usalama wa wanahabari kwa sasa uko hatarini kama inavyojionyesha.

DW ilimhoji Nchimbi kufuatia tukio la kinyama la kutekwa na kujeruhiwa kwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania, Absalom Kibanda, ambaye pia ni mhariri mtendaji wa Habari Co-operation.

Tukio hilo ambalo Nchimbi anataka kulijengea hoja ili lionekane ni la kawaida katika jamii ya Watanzania, limekuja baada ya matukio kadhaa ya mashambulizi yaliyolengwa kwa makusudi kwa wanahabari. Matukio ya karibuni yakiwa ni pamoja na kuvamiwa kwa ofisi za gazeti la Mwanahalisi, ambako mhariri mtendaji wa gazeti hilo, Saidi Kubenea, pamoja na mshauri wa taaluma, Ndimara Tegambwage, walijeruhiwa na watu wasiojulikana.

Mbali na tukio hilo likafuatia tukio lingine la kushambuliwa kwa mwanahabari, Daudi Mwangosi, na watu wanaojulikana, tena wa vyombo vya usalama wa raia, ambapo mwanahabari huyo aliyekuwa anatekeleza majukumu yake alipoteza maisha baada ya kulipuliwa na bomu lililoelekezwa tumboni kwake chini ya usimamizi wa Kamanda wa Polisi wa mkoa Iringa, Michael Kamuhanda.

Baada ya tukio hilo la kijijini Nyololo, Mfindi, Iringa, likafuatia tukio la mwanahabari Shabani Matutu kuvamiwa nyumbani kwake, Kuduchi Machimbo, nje kidogo ya jiji la Dar es salaam,  na kikosi cha wanausalama waliomjeruhi kwa risasi begani kwa visingizio visivyo na mashiko.

Matukio hayo yasiyolenga kwenye kitu kingine zaidi ya uhai wa mtu tunawezaje kuyachukulia ni ya kawaida tukiwa tumeyafananisha na matukio ya vibaka?

Tulizoea ujambazi unaolenga kwenye mali, lakini ujambazi unaolenga tu kwenye uhai wa mtu tunawezaje kuuita ni wa kawaida? Mali inaweza ikaporwa na ikapatikana nyingine, lakini uhai unapoporwa unawezaje kupatikana mwingine? Je, Mheshimiwa Nchimbi tukubali hii ni kawaida?

Na kwa nini ujambazi huu uchague taaluma? Tuuchukulie unakuja kama ajali, lakini mara zote ajali hizo ziwakute wanahabari tu! Dukuduku langu lingepungua kama mashambulizi haya ya kinyama yangekuwa yanaelekezwa kwa watu wa taaluma mbalimbali bila kuiandama taaluma moja tu.

La muhimu ninalotaka kukumbusha na kuhoji ni kwamba Waziri Nchimbi anayo dhamana ya mambo ya ndani ya nchi yetu. Chini yake ndiko kuna Jeshi la Polisi ambalo lipo kuulinda usalama wa raia, na kwahiyo jeshi hilo likajulikana kwa kifupi kama Usalama wa Raia.

Kutokana na kuwepo wa jeshi hilo wananchi wanapaswa kutembea wakijidai bila hofu wakijivunia uwepo wa jeshi lao hilo. Ndiyo maana wanalipa kodi ili kodi hizo, pamoja na mambo mengine, zihakikishe chombo hicho kinabaki imara kuwakikishia usalama wao.

Kwahiyo kinachotarajiwa na wananchi kutoka kwenye chombo hicho ni habari za kuyazima matukio yoyote ya uhalifu yanayokuwa yamepangwa kutekelezwa na wahalifu dhidi ya raia wema na mali zao.

Jambo la kusikitisha ni kwamba mambo yamekuwa kinyume chake katika siku za karibuni hapa nchini. Uhalifu limegeuka jambo la kawaida hapa kwetu. Wananchi wanadhurika na wengine kupoteza mali zao au vyote viwili. Chombo kilichopaswa kuwahakikishia usalama, wao na mali zao,  kinajigeuza chombo cha kufanya uchunguzi kana kwamba hakihusiki na ulinzi wa usalama!

Kila baada ya tukio la uhalifu chombo kilichopaswa kuhakikisha uhalifu hautendeki ndicho kinajipa jukumu la kuchunguza kwa nini uhalifu umetendeka na umetendekaje! Wakati uhalifu umeishafanyika na madhara yasiyoponyeka yameishatokea, chombo cha usalama kinahangaika na uchunguzi!

Na yumkini chombo cha kulinda uhalifu usitokee kinapojigeuza cha kuchunguza,  uhalifu unapata mvuto sababu unakuwa hauna kinga, utafanyika ili baadaye ukachunguzwe.

Swali la muhimu la kujiuliza ni kwamba Jeshi la Polisi ni kwa ajili ya kuulinda usalama wa raia au ni la kufanya uchunguzi kila baada ya usalama wa raia kutibuka?

Je, wananchi wanapaswa waishi kwa kuutegemea usalama wao na mali zao au kwa kuutegemea uchunguzi unaofanyika baada ya kuwa wamedhurika? Tulitegemee Jeshi la Polisi katika lipi? Kuulinda usalama wetu na mali zetu au kutufanyia uchunguzi wakati baadhi yetu wamepoteza mali na hata maisha?

Absalom Kibanda ni kijana aliyekuwa buheri wa afya kabla ya usalama wake kuyeyuka na kujikuta ameangukia mikononi mwa majahili. Kwa sasa tayari afya yake ni mgogoro, akipona hawezi tena kurudia hali yake ya kawaida, na si ajabu akawa chongo kulingana na mashambulizi aliyofanyiwa na majahili hayo. Ni jambo linalouma sana.

Lakini tunaambiwa kwamba polisi wamejipanga kufanya uchunguzi wa “kufa mtu”! Je, baada ya uchunguzi huo wa nguvu Kibanda atarudia hali yake ya kawaida? Jicho lake litapona?

Kilichopaswa kufanywa na polisi ni kutumia walau moja ya miamoja ya nguvu inayotumika kufanya uchunguzi ili kuulinda usalama wake, sio kufanya uchunguzi wakati Kibanda kaishapoteza jicho na meno. Usalama wa raia si kusubiri raia adhurike au afe kusudi Jeshi la Polisi lionyeshe manjonjo yake katika uchunguzi, kinachopaswa kuangaliwa ni usalama kwanza. Raia asidhurike wala kufa katika mazingira yanayoweza kuepusha vitu hivyo.

Mfano, mwandishi mmoja anayeishi nchini Scotland, majuzi tu katueleza jinsi vyombo vya usalama vya wenzetu vinavyofanya kazi kwa ufasaha. Vyenyewe vinafanya uchunguzi kabla ya tukio lenye madhara na kuliepusha.

Alieleza jinsi polisi walivyokwenda nyumbani kwake alfajiri na kujitambulisha kisha wakamweleza kuwa anafuatiliwa na watu wasio wema kwake ili akachukue tahadhari. Polisi hao hawakutaka mtu huyo adhurike kwanza ndipo waanze uchunguzi wa nini kimemsibu.

Kwahiyo hata hapa kwetu ningetegemea polisi wamfuate Kibanda, au walau kumpigia simu, kumweleza kuwa usalama wake ulikuwa hatarini kusudi achukue tahadhari. Hapo ningeamini kwamba vyombo vyetu vya usalama kweli viko kazini na vinaitumia kwa umakini intelijensia yake kwa manufaa ya wananchi. Lakini sio ile intelijensia inayotumika tu kuzuia mikutano ya hadhara ya vyama vya upinzani.

Nimalizie kwa kukumbusha ya enzi za nyuma. Wakati wanahabari kwa sasa wanaonekana ni maadui kwa baadhi ya watumishi wa umma hasa walio katika vyombo vya dola, mfano kama RPC wa Iringa, Michael Kamuhanda, miaka ya nyuma wanahabari walikuwa vipenzi vya watu kama hao.

Katika Vita ya Kagera, 1978 – 79, Jenerali David Msuguri, akiwa Brigedia wakati huo, aliwapenda sana waandishi wa habari waliokuwa wanaripoti mwenendo wa vita kutokea uwanja wa mapambano kiasi cha kuwaita makomandoo wake. Hiyo ilitokana na wanahabri kutaka kufika katika kila eneo la tukio ili wakapate cha kuuhabarisha umma katika uhalisia wake. Wanahabari walifika hata mahali ambapo askari hawakuona umuhimu wa kufika zaidi ya kutuma salaamu za makombora. Wanahabari walifanya hivyo kwa kujitoa mhanga mpaka Msuguri akaona wanafaa kuitwa makomandoo. Walikuwa wanatimiza jukumu lao kwa moyo mmoja. Ukomandoo huo bado upo nap engine unaongezeka, lakini  je, kwa nini kwa sasa ukomandoo huo hauthaminiwi?

Nakutakia kupona kwa haraka ndugu yangu Komandoo Absalom Kibanda, pole sana. Wahaya wanasema “Bishanga abashaija”, yaani hayo huwakuta wanaume.


0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau