Bukobawadau

YA KCU (1990) LTD NI MAKUBWA KULIKO YANAVYOONEKANA .

Na Prudence Karugendo
PAMOJA na serikali kukiri kwamba matatizo yaliyomo kwenye Chama Kikuu cha Ushirika, mkoani Kagera, KCU (1990) Ltd., ni makubwa kuliko yanavyoonekana na kuthibitisha kwamba inayafanyia kazi kwa njia inazozijua yenyewe baada ya kuzishtukia mbinu chafu za wafanyakazi na viongozi wa chama hicho za  kuingilia mara kwa mara uchunguzi wa serikali unaofanywa dhidi ya tuhuma ndani ya chama hicho, pamoja na ahadi ya kwamba serikali inaunda tume itayojitegemea katika kuudhibiti uendeshaji wa vyama vya ushirika, bado wanachama wa KCU (1990) Ltd. wanayo mengi ambayo wasingetaka yabaki nyuma ya pazia.
Wanachama hao wanayo madai ya kwamba, mbali na ufisadi wa aina mbalimbali ambao wameishaupigia sana kelele kwenye chama chao,  kuna ufisadi unaofanyika  kupitia kwenye matengenezo ya magari ya chama chao hicho cha ushirika.
Inasemekana kwamba baadhi ya madereva wa KCU (1990) Ltd. waliandika barua kwa uongozi wa ushirika wakiomba kubadilishiwa sehemu ya kutengenezea magari (gereji) kwani uwezo wa sehemu waliyokuwa wakiitumia ulikuwa ni mdogo mno. Lakini eti uongozi haukufanya kitu chochote zaidi ya kuwasimamisha kazi madereva walioandika barua hiyo. Wapo madereva waliobambikiwa makosa, kama ya kuiba vifaa vya magari, katika kuhalalisha kuondolewa kwao kazini. Lakini sababu hasa ikiwa ni hiyo ya kuikataa gereji bubu kwa ajili ya kutengeneza magari ya chama cha ushirika.
Inasemekana pia kwamba mmiliki mmoja wa gereji inayolalamikiwa aliwahi kumuapia dereva mmojawapo kwamba atafanya kila njia ahakikishe anafukuzwa kazi.
Yapo madai mengine ya kwamba hayo yote yanatokea kwa vile Meneja Mkuu na baadhi ya wajumbe wa Bodi wamekuwa wakigawana pesa wanazodai ni za matengenezo ya magari.
Aidha,  inasemekana kwamba Meneja Mkuu anaoa nyumba moja na mmoja wa wamiliki wa gereji hiyo inayolalamikiwa kuwa mojawapo ya matundu yanayopoteza pesa za wanaushirika.
Kwa hali hiyo basi, bado chama cha ushirika, KCU (1990) Ltd.,  kimefanywa kiendelee kuonekana ni mali ya mtu binafsi na siyo chombo kinachowapa tija wakulima wa kahawa ambao ndio wamiliki wa chombo hicho.
Shutuma nyingine zinaelekezwa kwa Mwenyekiti wa Bodi ya KCU (1990) Ltd.. Inasemekana, kwa kawaida, mwenyekiti anatakiwa kufika ofisini mara mbili kwa wiki, kama ilivyokuwa ikifanyika miaka ya nyuma wakati chama hicho kilipokuwa kikiendesha shughuli zake kwa ufanisi na kuleta tija kwa wanaushirika, ili kufanya mambo yasiyokuwa ya muda wote ofisini kama vile kusaini hundi na kuangalia shughuli nyingine za kiutendaji.
Lakini baadaye, kutokana na kuhitajika mara kwa mara, basi ikaonekana ni bora mwenyekiti awe ofisini mara tatu kwa wiki, yaani Jumatatu, Jumatano na Ijumaa.
Lakini hatahivyo inasemekana mwenyekiti wa sasa amekuwa akienda ofisini kwa siku zote za wiki na kulipwa posho siku zote hizo. Mbali na hilo mwenyekiti anatumia gari la KCU (1990) Ltd. kumfuata nyumbani kwake, Muhutwe, Muleba,  kuja ofisini, Bukoba Mjini, na kumrudisha kwa umbari ambao ni kama kilometa 86 kwenda na kurudi.
Kwahiyo mwenyekiti huyo tangu aingie madarakani ameishatumia kiasi kisichopungua shilingi 65, 000, 000/= zilizolipwa kwake kama posho. Vilevile ametumia kiasi cha shilingi 68, 640, 000/= kama gharama ya mafuta ya gari linapomfuata na kumrudisha kwake mara tano kwa wiki tangu awe mwenyekiti. Hiyo haihusishi gharama za matengenezo ya gari linalotumika kwa ajili yake.
Hali hiyo imesababisha hadi akawekewa tangazo kwenye mlango wa ofisi yake angalau kumkumbusha siku anazotakiwa kuwa ofisini ijapokuwa utekelezaji wa tangazo hilo ni wa matata sana.
Shutuma nyingine ni kwamba chama kilinunua magunia ya kuwekea kahawa safi ambayo hayakuwa na ubora unaotakiwa na hivyo kulazimika kununua magunia mengine tena kwa ajili ya kusafirisha kahawa safi kwenda nje. Ikumbukwe kwamba yote hiyo ilifanyika bila kufuata taratibu za manunuzi, na pia bila kuhusisha wataalamu, na hivyo kukisababishia chama cha ushirika hasara ya takriban shilingi milioni 60.
Madai mengine ni kwamba Meneja Mkuu, kwa kutumia ubabe wake, alifanya mabadiliko katika utaratibu wa ulinzi wa mali za chama. Alibadilisha walinzi katika hoteli zinazomilikiwa na KCU (1990) Ltd, Lake na Bukoba Co-op. zilizopo Bukoba Mjini, pamoja na walinzi wanaolinda kwenye mradi wa kuosha kahawa wa Birabo wilayani Muleba, na kuwaweka walinzi wa kampuni yake mwenyewe ya Kamweruka Security. Kampuni hiyo ya ulinzi inamilikiwa na yeye Meneja Mkuu kwa kushirikiana na Afisa Ardhi na Majengo wa KCU (1990) Ltd.. Na kibaya zaidi ni kwamba kampuni hiyo haikupata zabuni yoyote wala mkataba wa ulinzi uliopitishwa na Bodi ya Wakurugenzi. Kampuni hiyo inafanya kazi kinyemela kwa maslahi yao binafsi yanayokinzana na ya kampuni ya Salu Security yenye mkataba halali wa kufanya shughuli za ulinzi kwenye mali za KCU (1990) Ltd..
Lakini inadaiwa kwamba yote hayo yanasababishwa na uongozi wa Bodi kutokuwa makini katika usimamizi mzima wa uendeshaji wa shughuli za ushirika. Eti inaonekana Mwenyekiti na Meneja Mkuu, kwa kwa makusudi mazima, wanafanya makosa hayo wakiamini kwamba hayawezi kujulikana kwa wanaushirika, ambao kwa asilimia iliyo kubwa ni wakulima wa vijijini wanaochukuliwa kuwa na uelewa mdogo wa mambo. Meneja Mkuu, mtu msomi, ndiye msimamizi mkuu wa shughuli za kila siku za chama cha ushirika.
Kwahiyo usomi wake unapaswa uwape faida kwa wakulima, ndiyo maana wakamuajiri,  na siyo kuwafilisi kwa vile eti wao hawajasoma na wana uelewa mdogo. Hivyo akautumia uelewa huo mdogo wa wanaushirika kama mtaji wa kujineemesha akiwa amejitajirisha kwa njia haramu.
Wanaushirika wanasema kwamba lenye uzito kwa watu hao wawili, Meneja Mkuu na Mwenyekiti, ni lile linalogusa kwenye maslahi yao binafsi tu basi.
Kwahiyo wanaushirika hao wanasema kwamba kwa vile Bodi ya Wakurugenzi imeshindwa kuleta amani na mshikamano ndani ya ushirika, basi vyombo vinavyohusika katika kushughulikia kadhia za aina hiyo vijaribu kuingilia kati angalau kuinusuru hali inayozidi kuwa tete kabla haijawa mbaya zaidi na ya kutisha.
Wanasema kwamba taarifa zilishapelekwa kwenye vyombo mbalimbali, ikiwemo Takukuru, lakini kwa mshangao wao wanasema hakuna chochote kilichofanyika, jambo linalowaletea hisia za kwamba kuna namna ya kupozana miongoni mwa wahusika kusudi mambo yabaki jinsi yalivyo.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau