Bukobawadau

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI MH. PROF. KULIKOYELA KANALWANDA KAHIGI (MB) KUHUSU MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA 2012/2013 NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA OFISI YA RAIS – MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014

UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 99(9) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, toleo la 2013, naomba kuwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA, kuhusu mapitio ya utekelezaji wa Bajeti ya 2012/2013 na makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA, kipindi hiki itajikita katika mambo machache mahususi katika Ofisi ya Rais - katika Utawala bora, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Mahusiano na Uratibu - ambayo tunayaona ni mapungufu. Lengo la kufanya hivyo ni  kuitaka Serikali ama ichukue hatua ya kuyatokomeza mapungufu hayo kwa kutangaza hadharani nia yake ya kuyakomesha, kisha ichukue hatua mwafaka, au ijiuzulu kwa kushindwa kuongoza dola.
  1. UTAWALA BORA 
2.1.      Idara ya Usalama wa Taifa – Ikulu
Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu sasa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA imeitaka Serikali kuwachukulia hatua maafisa wa Idara ya Usalama wa Taifa – Ikulu ambao wanatuhumiwa kujihusisha na vitendo vya kihalifu vya utekaji na utesaji kwa watu wanaoonekana kuikosoa Serikali, lakini mpaka sasa hakuna hatua dhahiri  zinazochukuliwa ilhali matukio hayo ya utekaji na utesaji yanazidi kuongezeka katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, aliyetajwa na Gazeti la Mwanahalisi kuhusika na kitendo cha kinyama cha kumteka na kumtesa Dkt. Ulimboka mwezi Juni, 2012 ni afisa wa Usalama wa Taifa, Ramadhani Ighondu Abeid. Tulitarajia Serikali, kupitia Jeshi la Polisi, ingemkamata na kumhoji mtu huyu ili kujiridhisha na tuhuma dhidi yake na kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria za nchi, lakini mpaka leo hakuna chochote kilichofanyika kuhusu uhalifu dhidi ya binadamu aliofanyiwa Dkt. Ulimboka, jambo ambalo linaashiria kwamba Serikali iliridhika na kilichotokea. Lakini jambo baya zaidi ni kwamba Gazeti la Mwanahalisi lililosaidia kugundua uhalifu huo lilifungiwa kwa muda usiojulikana.
Mheshimiwa Spika, mazingira ya kuteswa kwa Mhariri wa Shirika la Habari, ndugu Absalom Kibanda yanafanana sana na yale ya kutekwa na kuteswa kwa Dkt. Ulimboka. Aidha, aina ya utesaji (mfano kung’olewa kucha, meno na kutobolewa jicho) unafanana sana na aina ya mateso aliyopata Dkt. Ulimboka. Hivyo, ushahidi wa kimazingira unaonesha kwamba waliomteka na kumtesa Dkt. Ulimboka yumkini ni walewale waliomteka na kumtesa Absalom Kibanda au mawakala wao.
Mheshimiwa Spika, katika sakata la Dkt. Ulimboka, jeshi la polisi lilidai kuwa limemkamata mtu mmoja lililodai kuwa ni raia wa Kenya ambaye hatima ya kesi yake haijulikani mpaka sasa. Kwa tukio la Absalom Kibanda hadi sasa hakuna taarifa rasmi ya watu walioshtakiwa kuhusu uhalifu huu dhidi ya binadamu. Dkt. Ulimboka ambaye angeweza kutoa msaada kwa Polisi kuwakamata waliohusika na uhalifu huo, hajahojiwa mpaka leo ingawa katika kiapo chake alichokiandika mbele ya mwanasheria wake alimtaja afisa wa Usalama wa Taifa - Ikulu kuwa alihusika kumteka na kumtesa. Inashangaza sana kwa nini Serikali haijataka kutumia maelezo ya Dkt. Ulimboka mwenyewe kuwakamata wahalifu. Jambo jingine la kusikitisha ni kwamba kuna dalili za wazi kwamba suala la kutekwa na kujeruhiwa vibaya kwa Absalom Kibanda limesahaulika kabisa.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya Adhabu ya Tanzania (Penal Code), kuteka na kutesa ni makosa ya jinai. Ni aibu kwa Idara ya Usalama wa Taifa iliyokabidhiwa jukumu kubwa na la heshima kubwa la kuulinda usalama na usitawi wa nchi kutuhumiwa kujihusisha na vitendo vya kikatili kama hivi. Kitendo cha kuhisiwa tu kwamba chombo hiki cha usalama kinajihusisha na vitendo vya kijinai moja kwa moja kinakikosesha sifa ya kufanya kazi ya usalama wa taifa. Na kwa kuwa chombo hiki kiko chini ya mamlaka ya Rais moja kwa moja  tayari ni doa kubwa kwa  Rais mwenyewe, Serikali yake na hata kwa chama chake.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ujasusi na Usalama ya Tanzania (Tanzania Intelligence and Security Services Act) ya 1996, Idara ya Usalama wa Taifa hairuhusiwi kufanya upelelezi wa ufuatiliaji - “ushushushu” kwa watu wanaoipinga  Serikali kwa misingi ya kisheria na kikatiba (kwa maana ya vyama vya siasa, vyombo vya habari na wanaharakati). Ibara ya 5(2), kipengele ‘a’ na ‘b’ inasomeka hivi:
              “It shall not be the function of the Service :      
a)    to enforce measures for security or;
b)   to institute surveillance of any person or category of persons  by reason only of his or their involvement in lawful protest or dissent in respect of any matter affecting the constitution , the laws or the Government of Tanzania”.
Mheshimiwa Spika, kwa tafsiri isiyo rasmi, sheria inasema hivi:
“Haitakuwa kazi ya Idara kufanya yafuatayo:
a)    kutekeleza hatua za usalama, au
b)   kufanya upelelezi wa ufuatiliaji wa mtu yeyote au kundi lolote la watu kwa sababu tu ya kuhusika na kupinga au kushiriki maandamano halali kuhusiana na jambo lolote la kikatiba, sheria au Serikali ya Tanzania”.
Mheshimiwa Spika, nimelazimika kunukuu sheria hii kwa kuwa Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA, inao ushahidi kwamba maafisa wa Usalama wa Taifa wamekuwa wakifanya upelelezi wa ufuatiliaji (surveillance) kwa watu wanaoipinga Serikali kwa misingi ya Katiba na sharia - jambo ambalo ni  kinyume na sheria iliyopo.
Mheshimiwa Spika, ushahidi wenyewe ni kwamba baada ya  Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama  wa CHADEMA kutuhumiwa kwamba  anahusika na ugaidi na video yake kurushwa kwenye mitandao ya kijamii, Muhidin Issa Michuzi, ambaye ni mpiga picha wa Rais, Ikulu, aliandika barua-pepe kwa Salvator Rweyemamu, Prosper Mbena, Hamis Mwinyimvua, Liberatus Mulamula, Msafiri Marwa, Laurent Ndumbaro na wengine ambao ni watumishi wenzake wa Ofisi Binafsi ya Rais akiwapongeza kwa kazi nzuri na ya ziada waliyoifanya ya kutengeneza video ya Lwakatare, na kuwaeleza  kuwa hiyo ni kete kubwa  kwao hivyo lazima waipigie kelele sana.
Mheshimiwa Spika, kuna ushahidi mwingine kwamba baadhi ya maafisa wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) wanawahonga kwa kuwalipa fedha watumishi wa CHADEMA ili watoe ushahidi wa uongo dhidi ya kesi inayomkabili Mkurugenzi wa Ulinzi na usalama wa CHADEMA. Miongoni mwa maafisa hao ni Sinbard Mwagha. Huyu ni ni afisa usalama wa taifa anayefanya kazi makao makuu ya idara hiyo. Taarifa zilizopo ni kwamba ndiye anayetumika kuendesha michezo ya kuhonga wanasiasa wa CCM na upinzani, na kwamba ndiye anayehusika pia   kuwapanga wabunge wa CCM waongee nini bungeni wakati wa vikao vya bunge kwa maslahi ya CCM.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya Adhabu (Penal Code), kutengeneza ushahidi wa uongo (fabrication of evidence) ni kosa la jinai na adhabu yake ni kifungo cha miaka saba gerezani. Hivyo, Kambi Rasmi ya Upinzani inalitaka Jeshi la Polisi kumkamata haraka sana Sinbad Mwagha ambaye tuna imani anafahamika na kumfungulia mashtaka ya kuhusika katika kutengeneza ushahidi wa uongo dhidi ya kesi inayomkabili Mkurugenzi wa Usalama wa CHADEMA, Ndugu Wilfred Lwakatare. Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa maelezo ya kina juu ya hatua ilizochukua hadi sasa dhidi ya maafisa wa usalama wengine ambao wanatuhumiwa kujihusisha na vitendo vya kihalifu.
Next Post Previous Post
Bukobawadau