Bukobawadau

KUTOKA JF HIZI NI Fikra Mbadala: # Lowassa kama Rais itakuwa ni Kikwete 2.0 (Marudio ya 2005)

Hawajakutana mtaani; wametoka mbali, na inajulikana kwa wengi kuwa safari yao kuelekea Magogoni ilikuwa na ahadi baina yao kuanzia 1995. Ushirika wao au Ubia wa uongozi wao ulikuwa wazi kuwa yeyote kati yao angeteuliwa kuwa Rais basi mwenzie angekuwa Waziri Mkuu. Matokeo yake Katiba ilifanyiwa mabadiliko 2005 ili kuhakikisha kuwa Waziri Mkuu anakuwa mtu wa tatu kuushika Urais katika Mnyororo wa Kufuatana kiuongozi (Rais, Makamu wa Rais halafu Waziri Mkuu). Kabla yake wa tatu kiuongozi alikuwa ni Spika. Bila ya mabadiliko yale Spika Sitta angekuwa anakaiumu Urais wakati wowote RAis na Makamu hawapo nchini.

Kashfa ya Richmond kama alivyosema Kikwete mbele ya wazee wa Dar ilikuwa ni "ajali ya kisiasa" tu kwa Lowassa. Ilikuwa ni ajali mbaya hata hivyo kwa sababu ilivuruga kwa kiasi kikubwa na imeacha ombwe kubwa sana la kujijenga tena Lowassa. Lakini halikufuta ndoto ya yeye kuutaka Urais; wengine wanaweza kusema ni "haki" yake; aliahidiwa kupokezana; anatoka Kikwete anaingia Lowassa.

Je, utawala wa Lowassa unaweza kuwa tofauti? Well, je nyani akiamua kuondoka shambani na kuwaachia ngedele mahindi yatakuwa salama? Kufikiria kuwa CCM chini ya Lowassa na Tanzania chini ya Lowassa itakuwa tofauti ni kujaribu kukinga mikono jangwani kungojea mvua.

Kwa ufupi, yeyote anayetaka mwendelezo wa utawala wa Kikwete kwa miaka kumi ijayo - ndani ya CCM na kwa taifa - uchaguzi uko wazi - kuhakikisha kuwa Lowassa anachaguliwa kuwa Rais. AU watu watuambie utawala wa Lowassa utakuwa na tofauti gani na utawala wa Kikwete na kwanini?
Next Post Previous Post
Bukobawadau