Bukobawadau

Lwakatare amwekea DPP pingamizi

Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare.

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare, amewasilisa pingamizi la awali dhidi ya maombi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), katika Mahakama ya Rufani.
DPP amewasilisha katika Mahakama ya Rufani maombi ya marejeo ya uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania wa kuwafutia washtakiwa hao mashtaka ya ugaidi, akiiomba mahakama hiyo iitishe majalada ya kesi hiyo na kuchunguza uhalali wa uamuzi huo.
Hata hivyo Lwakatare kupitia kwa jopo la mawakili wake, jana aliwasilisha pingamizi la awali dhidi ya maombi hayo akiainisha hoja mbili, ambazo mawakili wake watazitoa wakati wa usikilizwaji wa maombi hayo.
‘‘Maombi hayo ya marejeo yana dosari ambazo haziwezi kurekebishwa kwa kutokana na kushindwa kuambatanisha nakala ya mwenendo ambao ndio maombi hayo yamejengwa.’’ anadai Lwakatare.
Katika hoja ya pili anadai kuwa kiapo kinachounga mkono maombi hayo ya marejeo, kina dosari ambazo haziwezi kurekebishika kwa kuwa kimehusisha na mambo mengine yasiyohusika.
Lwakatare na Rwezaura walikuwa wakikabiliwa na mashtaka manne, matatu kati yake yakiwa ya ugaidi na moja la kawaida la jinai, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakidaiwa kula njama na kupanga kumteka Dennis Msacky na kisha kumdhuru kwa kutumia sumu.
Hata hivyo, Mei 8, mwaka huu Jaji Lawrence Kaduri wa Mahakama Kuu aliwafutia mashtaka hayo matatu ya ugaidi na kuwabakizia shtaka moja linaloangukia kwenye jinai ya kula njama za kutenda kosa la kumdhuru Msacky kwa kutumia sumu.
Jaji Kaduri alifikia uamuzi huo kutokana na maombi yaliyowasilishwa kwake na mawakili wa washtakiwa hao, wakipinga uamuzi wa DPP kuwafutia mashtaka katika kesi ya awali, namba 37, ya mwaka 2013 na kisha kuwakamata na kuwafungulia tena kesi yenye mashtaka hayohayo muda mfupi baadaye.
Kutokana na uamuzi huo wa Mahakama Kuu, ndipo DPP alipowasilisha maombi ya marejeo katika Mahakama ya Rufani.
Katika maombi hayo DPP pia anaiomba Mahakama ya Rufani ifute uamuzi na amri za Mahakama Kuu,kuhusu uhalali wa mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili washtakiwa, akidai kuwa Mahakama Kuu haikuwa sahihi.
Next Post Previous Post
Bukobawadau