Bukobawadau

Kagame ana lake jambo- wasomi


Dar es Salaam.Siku moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kuzungumzia mgogoro uliojitokeza baina yake na Rais wa Rwanda, Paul Kagame baadhi ya wasomi nchini wamesema Kagame ana kitu kimejificha ndani moyo wake.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam jana, wasomi hao walisema kitendo cha Rais Kikwete kutoa ushauri na Rais Kagame kukasirika, inaonekana wazi kuwa kuna kitu kimejificha.
“Haiwezekani mtu akupe ushauri halafu ukasirike, lazima kutakuwa na kitu kimejificha ndani ya moyo wa Kagame, hivyo basi anapaswa kukizungumza ili kupunguza mgogoro ambao unaweza kujitokeza,”alisema Profesa Gaudence Mpangala wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM).
Aliongeza, historia ya Rwanda inaojionyesha wazi kuwa, wameingia kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyosababisha idadi kubwa ya watu kufariki, hivyo basi wanapaswa kuwa makini na kujiepusha na matatizo mengine ambayo yanaweza kusababisha migogoro.
Alisema, kauli ya Rais Kikwete si mbaya, bali inaleta sura mpya baada ya kukaa kwenye meza moja na kujadili migogoro iliyopo,ili kupata ufumbuzi, jambo ambalo linaweza kupunguza ukubwa wa tatizo.
Naye Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,(UDSM), Bashiru Ally alisema Rais Kikwete amewafungua macho Watanzania waliokuwa hawajui chochote kinachoendelea baina ya nchi hizo mbili.
Aliongeza kuwa Rais Kikwete alijaribu kufafanua tatizo lililopo na kuonyesha hali halisi ya uhusiano wa nchi hizo mbili ili usiweze kuleta uhusiano mbaya, jambo ambalo linaweza kusababisha matatizo.
Alisema, kutokana na hali hiyo Kagame anapaswa kutekeleza ushauri huo au kuuacha na si kuendelea kutoa lugha za matusi ambazo zinaweza kuchochea migogoro.
Next Post Previous Post
Bukobawadau