Bukobawadau

TAARIFA YA KUTANGAZA FURSA ZA UWEKEZAJI MKOANI KAGERA KWAAJILI YA KUCHAPISHWA KWENYE TOLEO MAALUM LA MKOA WA KAGERA

Jiografia ya Mkoa wa Kagera


Mkoa wa Kagera upo Kaskazini Magharibi mwa nchi ya Tanzania na unapakana na nchi
za Uganda kwa upande wa Kaskazini, Rwanda na Burundi kwa upande wa Magharibi,
mikoa ya Kigoma na Shinyanga kwa upande wa Kusini. Mikoa ya Geita na Mwanza kwa
upande wa Kusini Mashariki. Mkoa wa Kagera ni daraja la nchi kavu kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na nchi za  Maziwa Makuu.


Eneo la mkoa, Mkoa wa Kagera una eneo la kilomita za mraba 35,685 kati ya hizo kilomita za mraba 28,513 ni eneo la nchi kavu ambalo ni sawa na asilimia 80 ya eneo lote la mkoa
na kilomita za mraba 7,172 ni eneo la maji sawa na asilimia 20.

Mkoa una visiwa vikubwa katika ziwa Victoria ambavyo ni Bumbire, Iroba, Ikuuza, Muhutwe na visiwa vingine vidogo vipatavyo 24. Mwinuko wa nchi (altitude) ni kati ya mita 1,100 na 1,800 juu ya usawa wa bahari.
Kiutawala mkoa umegawanyika katika wilaya saba (7) ambazo ni Biharamulo, Bukoba,
Karagwe, Kyerwa, Missenyi, Muleba na Ngara. Mkoa una Halmashauri za wilaya 7 na ya
Manispaa moja (1), Tarafa 29, Kata 181, Vijiji vilivyosajiliwa 640, mitaa 66 na Vitongoji
3,712. Aidha, mkoa una majimbo tisa (9) ya uchaguzi.
Misimu ya Mvua; Mkoa wa Kagera unayo misimu miwili ya mvua za vuli na za masika
kutokana na kuwa na sifa za ukanda wa ikweta, mvua hizo ni za miezi ya Machi – Juni na
Septemba – Desemba, kwa wastani wa 500 – 2000 mm kwa mwaka. Mvua ni nyingi
pembezoni mwa maeneo ya Ziwa Victoria hususani katika wilaya za Bukoba na Missenyi.
Joto la wastani kwa maeneo mengi ya mkoa wa Kagera ni kati ya 20°C - 28°C.
Idadi ya watu na Uchumi wa Mkoa
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, Mkoa wa Kagera una idadi ya
watu wapatao 2,458,023,
Kutokana na kuimarika kwa miundombinu na uwekezaji ulioanza kufanyika mkoa wa
Kagera, uchumi wa mkoa umeendelea kuimarika na unatoa mchango wa ajira kwa vijana na
kuchangia kuongezeka kwa pato la mkoa kutoka shs. millioni 1,488,061 (2011) hadi shs.
millioni 1,760,458 (2012) huku pato la mwananchi nalo likipanda kutoka shs. 559,070 (2011)
hadi shs. 716, 209 (2012)
HALI NA FURSA ZA UWEKEZAJI MKOA WA KAGERA:
Hali ya uwekezaji:
Uwekezaji ni chanzo cha maendeleo endelevu, ukuzaji ajira, ongezeko la kipato na
upunguzaji umasikini kwa wananchi. Mkoa wa Kagera umekuwa na mikakati mbalimbali ya
kuvutia wawekezaji kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo pamoja na Mamlaka
ya Serikali za Mitaa mkoani Kagera.
2
Juhudi hizo zimeanza kuzaa matunda kwa wawekezaji kuanza kujitokeza kuwekeza katika
sekta mbalimbali mkoani Kagera. Wawekezaji hao wanaendelea kuonyesha ushirikiano wa
karibu kati yao na Serikali katika ngazi mbalimbali.
Fursa za uwekezaji mkoani:
Jiografia ya mkoa wa Kagera, Fursa kubwa na ya pekee ya mkoa wa Kagera ni nafasi
yake ya kijiografia kwa kupakana na nchi za Uganda kwa upande wa kaskazini, Rwanda na
Burundi kwa upande wa Magharibi, Kenya kwa upande Ziwa Victoria na pia kuwa jirani na
nchi za Kongo DRC na Sudan Kusini. Nafasi hii ya mkoa inafanya wawekezaji
watakaopenda kuja kuwekeza katika mkoa wa Kagera kuwa na fursa ya masoko ya nchi
jirani na pia kupata malighafi kutoka nchi hizo. Watafaidika sana na soko la pamoja la
Afrika Mashariki (East African Common Market)

Hali ya hewa nzuri, Kufuatia Mkoa wa Kagera kuwa na misimu miwili ya mvua za vuli na za
masika na pia kuwa na sifa za ukanda wa Ikweta, shughuli nyingi za kilimo za mazao
mbalimbali ikiwemo kahawa, migomba, pamba, tumbaku, miwa, mahindi, mpunga, mihogo,
viazi, vanila na mazao mengine zinaweza kufanyika.
Ardhi yenye rutuba, Mkoa wa Kagera una bahati ya kuwa na ardhi nzuri yenye rutuba
inayofaa kwa kilimo na ufugaji. Ardhi hii inastawisha karibu mazao yote ya chakula na
biashara na pia maeneo mengine yanafaa ufugaji wa kisasa wa mifugo. Wilaya zote
zimeainisha maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wawekezaji mahiri (potential investors).
Kilimo, Sekta ya kilimo ambayo ndiyo chachu ya ukuaji wa uchumi katika Mkoa wa Kagera
bado haijawekezwa ipasavyo pamoja na kuwa na maeneo ya kutosha (kama bonde la mto
Ngono, bonde la Burigi ). Aidha, kuwepo na maeneo yanayofaa kwa umwagiliaji unafanya
mkoa wa Kagera kuwa na mvuto wa pekee.
Uwepo wa miundombinu imara, Kufuatia mkoa kuwa na jumla ya kilometa 7,244.65 za
barabara ikiwemo kilometa 5,330.31 zilizo chini ya Halmashauri za Wilaya na Manispaa,
Kilometa 1,914.34 za barabara kuu na za Mkoa zilizo chini ya Wakala wa Barabara
TANROADS. Kati ya hizo kilometa 639.11 ni barabara za lami, kilometa 3,050.74 ni
barabara za changarawe na kilometa 3,554.90 ni barabara za udongo, zinafanya mkoa
mzima kupitika kiurahisi mwaka mzima. Barabara hizi zinaunganisha Mkoa na nchi jirani na
mikoa jirani pia
Mbali na kuwa na mtandao mzuri wa barabara, Mkoa wa Kagera una kiwanja kizuri cha
ndege cha Bukoba kilichoboreshwa kwa kuwekewa lami na hivyo kuwezesha ndege kutua
wakati wote. Pia kuna usafiri wa kuaminika wa meli toka Bukoba kwenda Mwanza.
Miundombinu hii, inapunguza gharama za usafiri na usafirishaji wa bidhaa katika uzalishaji
na kufanya bidhaa zinazozalishwa kuwa na uwezo mkubwa wa kushindana katika masoko.
Uchimbaji Madini, Mkoa una maeneo yenye madini mbalimbali ambayo yanafaa
kuwekezwa ili kuchangia kukua kwa pato la mkoa na taifa. Maeneo ambayo hupatikana
madini ni pamoja na Tulawaka (Biharamulo) ambako huchimbwa dhahabu, Kabanga
(Ngara) ambako hupatikana madini ya “nickel” na Kyerwa ambapo hupatikana madini aina
ya bati. Aidha, yapo pia maeneo ya fukwe za Ziwa Victoria ambako hupatikana nchanga
mzuri unaofaa kutengeneza vioo na bidhaa zake.
3


Utalii, Mkoa una maeneo ya mbuga yanayohifadhiwa na Serikali ambayo yakitumiwa vizuri
kwa uwekezaji yataongeza tija ya ukuaji uchumi ndani ya mkoa na kwa watu binafsi. Baadhi
ya maeneo haya ya mbuga za uwindaji ni pamoja na mapori ya hifadhi ya Burigi,
Biharamulo na Ibanda. Wanyama wanaohifadhiwa katika mapori hayo ni kivutio kikubwa
cha utalii.
Vivutio vingine ni pamoja na maporomoko ya maji Rusumo, Bugonzi na Kyamnene, ufukwe
wa ziwa Victoria, mto Kagera, msitu wa Minziro (bainouai), visiwa vya Bumbile, Kerebe,
chemichemi ya maji moto - Karagwe pamoja na utalii wa utamaduni (Cultural Tourism)
kulingana na mila na desturi za makabila yaliyopo Mkoa wa Kagera.
Uwekezaji katika ziwa Victoria, Ziwa Victoria linafaa kwa uwekezaji lakini halijaweza
kutumiwa kikamilifu na kuchangia pato la mkoa. Katika Ziwa Victoria, shughuli za usafiri
kupitia Ziwa hili ni wa kiwango cha chini. Usafiri huo kama ukiboreshwa utaweza kuinua na
kuchangia kukua kwa uchumi wa mkoa na uwekezaji. Usafiri wa meli ungeweza kutoka
Bukoba, Mwanza, Musoma, Kisumu, Jinja, Entebbe na kurudi Bukoba.
Ufugaji nyuki, Mkoa wa Kagera unakadiriwa kuwa na misitu (Hifadhi na mataji wazi) na
mapori vyenye jamii mbalimbali za miti kama vile miyombo, podo, misambya, mininga na
miemezi kwenye eneo la kilometa za mraba 10,148 sawa na asilimia 35 ya eneo la nchi
kavu. Hii ni fursa nzuri ya ufugaji nyuki katika misitu na mapori hayo.
Ufugaji Mifugo, Uwekezaji unafaa katika ranchi ndogo na za kati za mifugo, viwanda vya
kusindika mazao ya mifugo kama vile nyama, mapambo, mifuko, viatu na mikanda kwa
kutumia ngozi, pembe na kwato za wanyama.
Maliasili, Uwekezaji katika mabwawa ya kufuga samaki (maziwa,mito mingi). Uwekezaji
katika Viwanda vya kutengeneza mitego ya kuvulia samaki inayokidhi viwango vya kisheria
na usindikaji wa dagaa (dagaa wengi sana). Uwekezaji katika mashamba ya miti hususan
miti ya asili ya matunda na Usindikaji wa matunda na mazao ya miti.
Ujenzi wa Miundombinu ya Elimu, Mkoa unahitaji uwekezaji katika elimu hasa katika
ujenzi na uendeshaji wa Vyuo vya Ufundi na Vyuo Vikuu. Mkoa kwa sasa una matawi vya
Vyuo Vikuu vitatu; Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, SAUT na Chuo cha Josia Kibira. Aidha
mkoa una vyuo vya ufundi thelathini (30). Kati ya hivyo saba (7) ni vya Serikali, viwili (2) ni
vya jumuia na ishirini na moja (21) ni vya mashirika au watu binafsi.
Idadi hii bado ni ndogo na tunahitaji iongezwe. Mkoa wa Kagera unatoa wastani wa
wanafuzi 48,000 wanaomaliza darasa la saba; wanafunzi 18,000 wa kidato cha nne na
wastani wa wanafunzi 2,000 wanaomaliza kidato cha sita kila mwaka. Hali hii inayofanya
kuwepo kwa mahitaji ya vyuo hivi ambavyo vitapunguza gharama ya usafiri na malazi kwa
wanafunzi wanaotoka maeneo ya jirani.
Ujenzi wa miundombinu ya Afya, Pamoja na mkoa kuwa na Zahanati 269, Vituo vya afya
30 na Hospitali 15 kwa mwaka 2013, bado mkoa unahitaji kuongeza huduma ya afya kwa
wananchi ili ifikiwe kwa urahisi na ubora zaidi. Hivyo tunakaribisha watu binafsi, mashirika
ya dini na Asasi mbalimbali za kiraia kuwekeza katika eneo hili.

Aidha, Serikali mkoani Kagera inaendelea kutoa wito kwa wawekezaji mbalimbali kuja
kuwekeza mkoani hapa pia inatambua mchango wa wawekezaji waliopo na tayari
wameanza kuwekeza kama ilivyobainishwa hapa chini.
Viwanda vya kusindika mazao ya kilimo, Sukari Kiwanda Sukari cha Kagera, Chai,
Kiwanda cha Chai cha Kagera, Kahawa, Kiwanda cha Kahawa cha TANICA na BUKOP,
kiwanda cha kahawa cha Amir Hamza, Kiwanda cha Kahawa cha Karagwe (Karagwe
Coffee Marketing Company), Ngara Farmers, Vanilla, Kiwanda cha wakulima Mayawa na
Maruku Vanilla
Viwanda vya kusindika samaki, Kiwanda cha Vicfish na Kagera Fish; eneo hili la
uwekezaji lina changamoto ya kutumia uvuvi wa kisasa
Viwanda vya vinywaji, Mali juice, Kiwanda cha Maji cha Kabanga na kiwanda cha maji
Asilia cha Bukoba na Bunena
Vitalu vya Madini, Kitalu cha dhahabu cha Tulawaka na Kiwanda cha nikeli cha Kabanga.
Kiwanda cha kusindika nyama, Kuna kiwanda kimoja cha kusindika Nyama - Agro Ranch
Hoteli za Kitaalii Walkgard Hotel, Kolping Hotel, Smart Hotel, Victorious Hotel na Bukoba
Cooperative Hotel
Hitimisho, Mkoa wa Kagera unaendelea kudumisha amani na utulivu ili kujenga mazingira
mazuri kwa wananchi na wadau wa maendeleo kuwekeza na kutekeleza shughuli
mbalimbali za maendeleo ya kiuchumi na kijamii bila kuwa na vikwazo vyovyote.
Tunawakaribisha wawekezaji wote kutoka ndani ya mkoa wa Kagera, ndani ya nchi na nje
ya nchi ya Tanzania kuwekeza katika mkoa wa Kagera.
Wawekezaji wanahakikishiwa Amani na Usalama, ushirikiano, mazingira yaliyoboreshwa ya
kufanyia biashara pamoja na miundombinu imara huku wakipata masoko yaliyo karibu
katika nchi za Afrika Mashari na Maziwa Makuu.
Kaulimbiu ya Mkoa: ‘Kagera! Kazi, Amani na Maendeleo’
‘Kazi, Amani na Maendeleo! Kagera’

Next Post Previous Post
Bukobawadau